in ,

Tanzania yaidhinishiwa mikopo yenye thamani ya trilioni 2 kutoka IMF

Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF) limeidhinisha mikopo yenye thamani ya dola milioni 935.6 [TZS trilioni 2.45] kwa Tanzania ili kusaidia mageuzi ya kiuchumi na kupunguza athari za mabadiliko ya tabianchi.

Mkopo wa dola milioni 786.2 [TZS trilioni 2] utatolewa kwa Tanzania kwa kipindi cha miezi 23 kupitia Mpango wa Ustahimilivu na Uendelevu (RSF) ili kusaidia jitihada za nchi kujenga ustahimilivu dhidi ya mabadiliko ya tabianchi.

Mkopo mwingine wa dola milioni 149.4 [TZS bilioni 392.2] utatolewa mara moja kupitia Mpango wa Mikopo ya Nyongeza (ECF), ambao unalenga kuimarisha urejeshaji wa kiuchumi, kuhifadhi utulivu wa kiuchumi wa jumla, na kuunga mkono ukuaji endelevu na shirikishi.

IMF imebainisha maendeleo yaliyofanywa na Tanzania katika kutekeleza mageuzi yanayohusiana na programu ya ufadhili, licha ya mazingira magumu ya kiuchumi ya kimataifa.

“Utendaji wa Tanzania chini ya programu ya mageuzi inayoungwa mkono na Mpango wa Mikopo ya Nyongeza (ECF) umekuwa imara. [..] Uwekezaji thabiti wa mamlaka katika ajenda yao ya mageuzi utabaki kuwa muhimu licha ya hatari za hali mbaya” amesema Naibu Mkurugenzi Mtendaji wa IMF, Bo Li.

Ameongeza kuwa “Uimarishaji wa kifedha unaoendana na ukuaji unaoendelea utasaidia kuimarisha uhimilivu wa kifedha na deni. Jitihada zinapaswa kuelekezwa katika kuongeza ukusanyaji wa mapato ya ndani na kuimarisha usimamizi wa fedha taslimu na udhibiti wa ahadi.”

Li ameeleza kuwa kuimarisha usimamizi wa fedha za umma na uwekezaji kutasaidia kudhibiti hatari za kifedha na kuboresha ufanisi wa uwekezaji wa umma.

Nchi 10 za Afrika zinazoongoza kutembelewa na watalii mwaka 2024

Mfahamu Askofu Wolfgang Pisa, Rais mpya wa Baraza la Maaskofu Katoliki