Joshua Nassari: Siwezi kumpinga Rais Magufuli

0
11

Aliyewahi kuwa Mbunge wa Arumeru Mashariki, Joshua Nassari amesema kuwa hawezi kumpinga Rais wa Tanzania, Dkt. Magufuli kwa kuwa ya mambo anayoyafanya ndiye aliyokuwa akiyapigia kelele wakati akiwa bungeni.

Nassari ameyasema hayo leo wakati akipokelewa rasmi ndani ya Chama cha Mapinduzi (CCM) mkoani Arusha ambapo amempongeza Rais Magufuli kwa mambo anayofanya ikiwamo kuiwezesha nchi kufikia uchumi wa kati.

Mwanasiasa huyo machachari amesema kuwa akiwa bungeni alikuwa akipigia kelele serikali kuboresha huduma za afya, elimu, miundombinu pamoja na kutatua migogoro ya ardhi ambayo serikali ya sasa imeyavalia njuga hayo yote.

Nassari amepokelewa ndani ya CCM leo na viongozi chama hicho mkoani humo ambapo amebainisha kuwa sababu kubwa iliyomfanya kujiunga CCM ni kuipenda sana nchi yake (Tanzania).

Mbali na Nassari wanachama wengine wa CHADEMA waliojiunga CCM leo ni pamoja na aliyekuwa Katibu wa Baraza la Vijana la CHADEMA (BAVICHA) ambaye amesema amejiunga chama hicho kwa ajili ya maslahi ya taifa, na sio kutaka uongozi wa cheo chochote.