Serikali yazuia halmashauri kutumia wafanyabiashara kutoa chanjo kwa mifugo

0
15

Serikali imeziagiza halmashauri kutotumia wafanyabiashara kuto chanjo kwa mifugo na kwamba halmashauri hizo zivunje mitakata ambayo zimeingia kwa ajili ya zoezi hilo.

Hayo yameelezwa na Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mashimba Ndaki akiwa ziarani ambapo baadhi ya wafugaji wamemlalamikia kuwa baadhi ya ng’ombe wao wamekuwa wakivimba na wengine kufa baada ya kupatiwa chanjo.

“Halmashauri zetu zote kuanzia sasa hivi ni marufuku kutumia wafanyabiashara kuchanja mifugo. Halmashauri zitumie wataalamu wa wizara ambao wamethibitishwa, hao wafanyabiashara kama mmeingia mikataba nao hiyo mikataba ivunjeni haraka iwezekanavyo hatuwezi kuchezea akili za watu namna hii.”

Waziri Ndaki akiwa ziarani amekataa kushuhudia zoezi la uchanjaji lililokuwa limeandaliwa baada ya kukasirishwa na uongozi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kishapu kutokuwa na takwimu yoyote ya idadi ya ng’ombe waliovimba na wengine kufa baada ya kuchanjwa.

Pia amemuagiza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kishapu kumuondoa mara moja kazini mhasibu wa halmashauri hiyo anayefanya kazi katika Mnada wa Upili wa Mhunze, Athanas Msiba kwa tuhuma za kutokuwa mwaminifu katika kuandika idadi ya mifugo inayoingia na kutoka katika mnada huo, hali inayosababisha wizara na halmashauri kukosa mapato stahiki.

Send this to a friend