Mchanganyiko wa maji ulivyosababisha vifo vya samaki Ziwa Victoria

0
26

Serikali imeeleza kuwa mwanzoni mwa mwezi Januari mwaka 2021, kulitolewa taarifa ya vifo vya samaki aina ya sangara katika Ziwa Victoria nchini Uganda, hasa katika maeneo ya Kaskazini Magharibi mwa nchi hiyo. Samaki waliokufa katika tukio hili ni aina ya sangara wakubwa.

Baada ya kufuatilia, serikali imesemea kwa upande wa
Tanzania, vifo hivi havijaripotiwa sehemu yoyote isipokuwa kwa wavuvi na wananchi wa eneo la Masonga – Sota, Tarime ambao walidai kuona vifo vya samaki siku ya Jumamosi Januari 2, 2021.

Hata hivyo maafisa uvuvi wa eneo husika hawakuona samaki waliokufa katika siku iliyotajwa na hata baada ya siku chache zilizofuatia.

Aidha, waliwasiliana na idara ya uvuvi nchini Uganda kufahamu kama samaki waliokufa nchini humo ni kwa sababu ya sumu na wakaelezwa kuwa samaki hao hawakufa kutokana na sumu.

Mamlaka ya Uganda imesema vifo hivyo vimetokana na tukio la kila mwaka linalotokana na mchanganyiko wa maji ziwani kati ya tabaka la chini lenye hewa ndogo ya Oksijeni na lile tabaka la juu.

Pamoja na kuwa vifo hivi havijaonekana kwenye maji ya upande wa Tanzania, wizara ya mifugo na uvuvi imesema kuna uwezekano kuwa mchanganyiko wa maji (mixing) ukafika Tanzania pia hasa kama hali ya hewa itaruhusu wakati wa mvua kubwa na upepo.

Wizara imesema ikionekama uwezekano wa kutomea vifo hivyo, hatua za haraka zitachukuliwa ili kubaini kama vinasababishwa na chanzo kilichozoeleka cha mabadiliko ya hali ya ziwa au vinatokana na shughuli za
kibinadamu ili hatua stahiki ziweze kuchukuliwa mapema.

Send this to a friend