Mambo ya kufahamu kuhusu chanjo ya Sinopharm inayoletwa nchini kutoka China

0
18

Septemba 2, 2021 Shirika la Afya Duniani (WHO) liliidhinisha matumizi ya muda ya chanjo dhidi ya UVIKO-19 ya Sinopharm kutoka China.

Serikali ya Tanzania inatarajia kupokea dozi milioni 2 mbili mwanzoni mwa Oktoba 2021 ikiwa ni mkakati wa kupambana na janga hilo linaloendelea kuiathiri dunia. Haya ni baadhi ya mambo unayotakiwa kufahamu kuhusu chanjo hiyo:

NANI ACHOMWE?
WHO haishauri watu wenye umri chini ya miaka 18 kutumia chanjo hiyo, na utafiti zaidi unaendelea kufanyika kuweza kubaini madhara yake kwa watu wenye umri huo.

Aidha, watu wenye mzio (Anaphylaxis/Allergy ) wa kitu chochote kilichopo kwenye chanjo hiyo hawatakiwa kutumia. Pia mtu mwenye joto la mwili lililozidi 38.5C wametakiwa kutokuchanjwa hadi hapo watakapokuwa na joto sawa au kupona homa.

WAJAWAZITO WACHANJWE?
Taarifa ambazo WHO inazo imeeleza kwa hazitoshelezi kubaini athari kamili zinazoweza kumpata mjamzito kutokana na chanjo hiyo. Hata hivyo shirika hilo limesema kuwa viambata vilivyotumika ni sawa na vinavyotumika kwenye chanjo nyingine ambazo zinatumika pia kwa wajawazito.

DOZI?
Chanjo hii inatolewa kwa dozi mbili ambapo WHO inashauri baada ya mhusika kuchomwa mara ya kwanza, asubiri kati ya wiki tatu hadi nne kabla kuchomwa mara pili. Endapo dozi ya pili itachomwa chini ya wiki tatu baada ya dozi ya kwanza, dozi hiyo haitohitaji kurudiwa. Endapo dozi ya pili itacheleweshwa kwa zaidi ya wiki nne, itatakiwa kutolewa haraka iwezekanavyo nafasi ikipatikana. Watu wote wanatakiwa kupata chanjo mbili.

ULINGANISHO NA CHANJO NYINGINE
Ni vigumu kulinganisha chanjo hizi kutokana na hatua tofauti zinazotumika katika utangenezaji wake, hata hivyo, chanjo zote ambazo zimeidhinishwa na WHO ni madhubuti kuzuia madhara makubwa ya UVIKO19 ikiwemo magonjwa nyemelezi na kulazwa.

Utafiti unaonesha kuwa inaweza kudhibiti maambukizi na kuuagua hadi kulazwa kwa asilimia 79.

INAZUIA VIRUSI VIPYA?
WHO imesema hakuna utafiti uliofanyika kuthibitisha endapo chanjo hiyo inadhibiti virusi vipya vya UVIKO19, na kwamba utafiti ukifanyika, taarifa zitatolewa.

INAZUIA KUAMBUKIZWA?
Hakuna taarifa toshelezi kuonesha kama ukichomwa chanjo hiyo hautoambukizwa au kusambaza UVIKO-19. WHO inaendelea kusisitiza matumizi ya barakoa, kunawa mikono kwa maji safi na salama, kukaa umbali wa mita moja au zaidi, kuepuka misongamano kama njia ya kudhibiti maambukizi.

CHANGAMOTO ZAKE?
Taarifa zinaonesha ‘side effects’ zilizoripotiwa zaidi kwa watu waliotumia chanjo hiyo ni maumivu ya kichwa, uchovu, na maumivu eneo ambapo umechomwa sindano.

Hadi Septemba 26 mwaka huu, jumla ya Watanzania 400,000 wamechomwa chanjo ambapo Julai mwaka hu Tanzania ilipokea zaidi ya dozi milioni 1 za chanjo ya Jansen kutoka nchini Marekani.

Send this to a friend