Linah azungumzia kiwango cha mahari yake

0
15

Mwanamuziki Lina Sanga (31) amefikisha miaka 11 kwenye muziki wa Tanzania, akiwa ni sehemu ya wasanii wachache wanaoendelea kufanya vizuri licha ya ukongwe wao.

Mwenyewe amesema kuwa siri ya kuendelea kufanya vizuri kwa muda wote ni pamoja na kutunga nyimbo nzuri hasa zinazoendana na soko la muziki kwa wakati huo, kukubali kukosolewa kwenye muzika wake pamoja na nidhamu.

Mbali na mafanikio hayo, mashabiki wa muziki nchini wamekuwa wakihoji kuhusu suala la ndoa, kwamba lini bibie huyo atafunga pingu za maisha.

“Ni majaliwa ya Mungu,” amesema msanii huyo kwa kifupi akimaanisha kuwa, Mungu akijalia, yeye hatokuwa na pingamizi.

Kuhusu mahari yake itakapofika wakati wa kuolewa amesema hawezi kujua baba yake atataka mahari ya shilingi ngapi kwani yeye ndiye mwenye mamlaka ya kutaja.

“Kiutamaduni sisi huwa hatutaji kiwango cha mahari, ni mzee ambaye anapanga,” amesema Lina ambye alitambulika kwenye anga ya muziki mwaka 2010.

Hata hivyo amesema kuwa amekuwa akipitia kipindi kigumu kutokana na kupata vishawishi vingi kutoka kwa wanaume ambapo vingi anaamini vimetokana na wengi kujua hajaolewa.

Mwanamuziki huyo kutoka mkoani Iringa ni mama wa mtoto mmoja aitwaye Tracey.