Wapinga adhabu ya kifungo kwa wanaokataa kuchanjwa

0
16

 

Mashirika ya kutetea Haki za Binadamu nchini Uganda yamepinga sheria ya kufungwa jela kwa watu watakaokataa chanjo katika milipuko ya magonjwa, adhabu ambayo inatajwa kufikia kifungo cha hadi miezi sita jela.

Muswada huo unalenga kuwachochea watu zaidi kujitokeza kuchomwa chanjo dhidi ya Ugonjwa wa Virusi vya Korona (UVIKO19) katika nchi hiyo, ambapo bado unakabiliwa na uwezekano wa kufanyiwa tathmini ya kina na kamati ya bunge inayohusika na masuala ya afya.

Aidha, Waziri wa Biashara wa Serikali ya Uganda wiki iliyopita alipendekeza marekebisho ya sheria ya afya ya umma ambayo itajumuisha faini au kifungo jela kwa wale ambao watakaidi kufuata hatua zilizowekwa na serikali ili kupambana na magonjwa ya kuambukiza.

Muswada huo unasema kwamba, yeyote anayeficha ugonjwa wa kuambukiza anaweza kukabiliwa na faini ya dola za Marekani 850, au kifungo cha hadi mwaka mmoja jela.

Hata hivyo, suala la kuwalazimisha watu kuchanjwa kabla ya kutumia usafiri wa umma nchini Uganda limepingwa na waendeshaji huduma hizo, huku taarifa kutoka kwa Waziri wa Afya wa Uganda, Dk. Jane Ruth Aceng Ocero mwezi uliopita akionesha zsidi ya chanjo 400,000 ziliharibiwa baada ya muda wake wa matumizi kumalizika bila kutumika.

 

Send this to a friend