Uganda: ‘Influencers’ kwenye mitandao ya kijamii kutozwa kodi

0
17

Mamlaka ya Mapato Uganda (URA) inatarajia ifikapo Juni 1, 2022 itakuwa na sera ya miamala ya kibishara inayofanyika kupitia intaneti, kama vile mitandao ya kijamii.

Kamishna Mkuu wa URA, John Musinguzi amesema kwamba tayari wamewasilisha sera hiyo Wizara ya Fedha wakiwa na matarajio kwamba itapitishwa na bunge na kuanza kutekelezwa kwenye mwaka wa fedha 2022/23.

Ametoa maelezo hayo katika mafunzo ya 10 ya mwaka kuhusu kodi kwa majaji wa Mahakama Kuu na wajumbe wa Mahakama ya Rufaa ya Kodi.

Katika mafunzo hayo Musinguzi aliwaomba wajumbe wa mkutano kutupilia mbali kesi 350 za kodi zenye thamani ya fedha za Uganda shilingi trilioni 1.2, ili fedha hizo ziweze kuingizwa kwenye mzunguko wa uchumi.

Hata hiyo Jaji Flavian Zeija alijibu kwamba watahakikisha kesi zinazohusiana na kodi zinapewa kipaumbele mahakamani.

Mwaka 2018 Uganda ilitangaza kuleta kodi ya matumizi ya mitandao ya kijamii ambapo mtumiaji angetakiwa kulipia kiasi TZS 116 ili kuweza kutumia mitandao mbalimbali ya kijamii ikiwemo Facebook, Twitter, na WhatsApp.

Hata hivyo baada ya muda mpango huo ulitupiliwa mbali baada ya lengo kutofikiwa na kupelekea kupungua kwa matumizi ya intaneti, badala yake ikaanzisha kodi ya 12% kwenye vifurushi vya intaneti.

Send this to a friend