Mume amfikisha mahakamani mkewe kwa kupeleka mshahara wake kanisani

0
16

Mwalimu wa shule ya Sekondari Jijini Mbeya, Julieth Kabuja (32) ameieleza Mahakama ya mwanzo Mkoani hapo kuwa ni bora ndoa yake ivunjike kuliko kumkabidhi mumewe kadi yake ya benki.

Ameyazungumza hayo mbele ya Mahakama ya mwanzo jijini hapo baada ya mumewe Charles Meshack (31) kufungua shauri la madai ya talaka akitaka kuachana na mkewe kwa kuhama dhehebu la katoliki na kuhamia la kilokole.

Aidha Meshack ambaye ni Askari Magereza amedai mkewe baada ya kuhamia katika ulokole fedha zake amekuwa akizipeleka kanisani kitendo kinachosababisha yeye kuzidiwa na majukumu ya familia.

“Naumia sana na majukumu, kodi ya nyumba nilipe mimi, ada za Watoto na chakula vyote mimi, halafu yeye mshahara wake apeleke kanisani, bora tuachane” alisema Meshack.
Hata hivyo Julieth aliiambia Mahakama kuwa yeye na mume wake wote ni wafanyakazi, lakini anashangaa anataka kumiliki kadi zote.

“Siku moja aliniamsha usiku na kuniambia nisipokubali kumkabidhi kadi yangu ya benki bora tuachane kwa kisingizio yeye alinilipia mahari hivyo mimi na kila kitu changu kipo chini yake, yaani kazi nifanye mimi halafu mshahara nimuachie huyu bwana, nipo tayari kuachika lakini siyo kuacha kadi yangu” alidai Julieth

Baada ya Hakimu Hafsa Shelimo kusikiliza pande zote mbili, aliahirisha kesi hiyo hadi Mei 12, mwaka huu kwaajili ya hukumu.

Send this to a friend