Wanawake wauawa, sehemu za siri zanyofolewa mkoani Mtwara

0
13

Mkuu wa Wilaya ya Masasi, Mkoa wa Mtwara, Claudia Kitta amesema wanawake watano wameuawa kikatili na watu wasiojulikana huku watatu kati yao wakinyofolewa sehemu zao za siri katika kipindi cha miezi mitatu.

Mkuu huyo amesema amesikitishwa na mauaji hayo na kusema kuwa ameshangazwa kwamba aina ya mauaji ni moja huku sababu zikiwa hazijafahamika, na kuongeza kuwa Jeshi la polisi linaendelea na uchunguzi.

“Inasikitisha kuona kwamba ndani ya miezi mitatu wanawake watano wamekutwa wameuawa katika maeneo tofauti. Hali hii inasikitisha na inatishia usalama wa wananchi,” amesema Kitta.

Ameongeza kuwa kamati ya ulinzi na usalama ya wilaya inaendelea kuimarisha ulinzi ili kuhakikisha matukio hayo yanakomeshwa, pia amewasihi wananchi kutoa taarifa polisi wanapowaona watu ambao hawawafahamu kwenye maeneo yao ili wafuatiliwe na kujua uhalisia wao.

Hata hivyo, Jeshi la polisi kupitia Kamanda wa polisi Mkoa wa Mtwara, Kamishna Msaidizi (ACP) Nicodemus Katembo limesema hadi sasa watu wawili wanashikiliwa na polisi kwa tuhuma za mauaji hayo.