Dodoma: Wazazi watoa rushwa watoto waachishwe shule wakafanye kazi za ndani

1
22

Baadhi ya wazazi katika Wilaya ya Chamwino mkoa wa Dodoma wamedaiwa kujaribu kutoa rushwa kwa waalimu ili watoto wao wafutwe shule kwa ajili ya kuchunga mifugo na kwenda mjini kufanya kazi za ndani.

Akizungumza Diwani wa Kata ya Idifu, Simon Kawea wakati wa kikao cha watumishi wa halmashauri hiyo ambacho mgeni rasmi alikuwa Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Anthony Mtaka amesema jamii ina tatizo la kutotambua umuhimu wa elimu.

“Mzazi anaona kumnunulia mtoto sare kwenda sekondari ni gharama kubwa, wazazi wengi hawatendei haki watoto katika jambo hili. Pia kuna wazazi wanaowaficha watoto siku ya mitihani, akiuliza anasema katoroka,” amesema Kawea.

Naye Mwenyekiti wa Kijiji cha Izava wilayani humo, Sokoine Mbelee amewatupia lawama wanasiasa na kudai kuwa hawasimamii maendeleo ya elimu, amedai mzazi akikamatwa kwa kosa la mtoto wake kutoripoti shuleni huwakingia kifua, jambo linalowakatisha tamaa watendaji.

Chanzo: Habari leo