BRELA kufuta kampuni 5,000

0
13

Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA) inakusudia kufuta kampuni 5,676 ambayo yameshindwa kukidhi matakwa ya sheria la kuwasilisha taarifa za mwaka kwa kampuni zilizosajiliwa hapa nchini.

Akizungumza na waandishi wa habari, Afisa Mtendaji Mkuu wa BRELA, Godfrey Nyaisa amesema zoezi hilo litafanyika kwa awamu ambapo awamu ya kwanza itajumuisha kampuni 5,676, kati ya hizo kampuni 5,284 zilisajiliwa hapa nchini, na kampuni 392 zilisajiliwa nje ya nchi na kupata hati ya utambuzi.

Amesema zipo kampuni zenye miaka zaidi ya 50 na hazina uthibitisho kuwa zinafanya biashara na hata kushindwa kuwasilisha taarifa za kila mwaka.

“Kifungu cha 438 kinazitaka kampuni ziliyosajiliwa nje ya nchi ambazo zina ofisi za biashara nchini kuwasilisha mizania (financial statement) ambapo kutokufanya hivyo kunatoa tafsiri kuwa kampuni hizo hazifanyi biashara hapa nchini,” amesema.

Ameongeza “Vifungu vya 400 na 441 vya sheria ya kampuni, vinanipa mamlaka mimi kama msajili wa makampuni kufuta makampuni ambayo hayafanyi biashara. Uwepo wa makampuni yasiyofanya biashara ni kinyume na sheria na mzigo kwa wakala wa kutunza kumbukumbu.”

Aidha, ameeleza faida ya kufungia kampuni hizo ni pamoja na daftari kubaki na kampuni ambazo ni hai, kupunguza changamoto ya upatikanaji wa majina ya kampuni na daftari kuwa na taarifa sahihi za makampuni.

Send this to a friend