Namna 5 bora za kumlinda mwanao dhidi ya hatari za mitandao ya kijamii

0
17

Mitandao ya kijamii inaweza kuwa mahali pazuri kwa kijana wako kufahamiana na familia, marafiki pamoja na kujifunza. Lakini pia inaweza kumpa mahudhui yasiyofaa pamoja na kuhatarisha usalama wake.

Hizi ni njia tano za kumlinda mtoto wako dhidi ya mitandao ya kijamii;

1. Zingatia umri:
Hakikisha haumruhusu mtoto wako kuwa na akaunti ya mitandao ya kijamii akiwa na umri mdogo kuliko umri unaotakiwa. Kwa Facebook, Twitter, Instagram na Snapchat, lazima awe na umri wa miaka 13 ili kujiunga. Ingawa YouTube inahitaji umri wa miaka 18, mtu aliye na umri wa miaka 13 anaweza kujisajili kwa ruhusa ya mzazi.

2. Weka mipaka:
Unapaswa kuzungumza na mwanao kuhusu uhalisia wa mitandao ya kijamii na namna ilivyo na madhara endapo itatumika vibaya. Weka mipaka kama vile picha gani anatakiwa kutuma na muda wa kuingia kwenye mtandao wa kijamii. Ni vizuri ukijua nywila [password] ili kujua akaunti ambazo amekuwa akizitembelea.

3. Kuwa mwangalifu na marafiki zake mitandaoni:
Mitandao ya kijamii inatumiwa na watu wazuri pamoja na watu wabaya, huwezi kujua yupi ni salama kwa mwanao pindi wanapomuomba urafiki. Hakikisha unamhimiza mwanao kuwa mwangalifu na watu asiowajua pamoja na kutotoa taarifa zake binafsi.

4. Jifunze lugha ya maandishi:
Mitandao ya kijamii huwa na lugha ya tofauti ili kuwasilisha jambo fulani hususani ujumbe wa ngono. Ni vizuri kama mzazi kuelewa lugha hizi ili uweze kumlinda mwanao dhidi ya picha na video zisizofaa kwa mtoto wako.

5. Muombe urafiki [m-follow]:
Mtoto wako anapokuwa na akaunti ya mtandao wa kijamii, muombe urafiki. Hii inaweza kukusaidia kufuatilia mtoto wako anafanya nini mtandaoni na anatuma picha za aina gani, vitu anavyopenda na hali anazozipitia kupitia machapisho [post] yake.

Send this to a friend