NIDA: Kitambulisho kikiisha muda unatakiwa kujaza fomu ya kuhuisha

0
27

Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA) imewatoa hofu Watanzania ambao vitambulisho vyao vinakwisha muda wa matumizi mwakani kuwa taarifa za utambulisho wao hazitapotea.

Msemaji wa NIDA, Geofrey Tengeneza amesema kumekuwa na maswali mengi na hofu miongoni mwa jamii kuwa vitambulisho vya Taifa vilivyotolewa mwaka 2012 ambavyo vitakwisha muda wake mwakani, taarifa zao zitapotea pia.

“Kwanza niwaondoe hofu wananchi, ni kweli kuwa vitambulisho vya taifa ambavyo vilianza kutolewa mwaka 2012 muda wake wa matumizi unaisha mwakani, lakini kinachoisha ni gamba tu kama ambavyo leseni ya udereva ina expire (kuisha muda) lakini taarifa za mtu hazipotei,” amesema Tengeneza.

Ameongeza kuwa wenye vitambulisho vinavyoisha muda mwakani, muda ukifika wanatakiwa kwenda kwenye ofisi za NIDA katika maeneo yao kupiga picha na kujaza fomu ya kuhuisha taarifa zao, kisha watasubiri maandalizi ya kupewa kitambulisho kingine chenye namba ile ile.