Watakaosoma Kiswahili vyuoni kupewa kipaumbele kwenye mkopo

0
11

Serikali imetenga TZS bilini 573 kwa ajili ya kutoa mikopo kwa wanafunzi wa elimu ya juu kwa mwaka wa masomo 2022/23, huku wanafunzi watakaosoma masomo ya lugha ya Kiswahili wakipewa kipaumbele.

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda akizungumza katika hafla ya kuzindua mwongozo wa uombaji wa mkopo kwa elimu ya juu amesema lengo la kutoa kipaumbele hicho ni kupata wakalimani wengi zaidi.

Lengo lingine ni kupata watu wanaoweza kuzungumza Kiswahili na Kiingereza kwa ufasaha pamoja na lugha nyngine za kigeni ili kukuza na kueneza lugha ya Kiswahili duniani.

Mbali na hayo, Mkenda amewahimiza waombaji mikopo ya elimu ya juu kwa mwaka 2022/23 kusoma na kuzingatia mwongozo uliotolewa na Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB), ili kuwasilisha maombi kwa usahihi.

Dirisha la kupokea maombi ya mikopo kwa njia ya mtandao linatarajiwa kufunguliwa Julai 19 hadi Septemba 30, 2022.

Send this to a friend