Mwanamke mjamzito abakwa na wanaume wanne

0
34

Mwanamke mmoja mjamzito mkazi wa Mtaa wa Joshoni Halmashauri ya Mji wa Njombe amebakwa na wanaume wanne akiwa amefungwa kitambaa mdomoni pamoja na kamba mikononi huku akitishiwa kuuawa endapo atapiga kelele.

Mwanamke huyo ameeleza kuwa tukio hilo lilitokea Julai 10, 2022 majira ya saa saba usiku nje ya nyumba anayoishi, huku wanaume hao wakihitaji fedha kabla ya kumfanyia ukatili huo.

“Nilikuwa nimelala nikasikia komeo inachezewa, nilipofungua mlango watu wanne wakaingia, wawili wakiwa wameshika panga na wawili wakiwa wameshika visu wakapekua kwenye pochi na kuchukua hela pamoja na simu iliyokuwa kitandani,” ameeleza.

Ameongeza kuwa baada ya kushindwa kuwapa kiasi kingine cha pesa walichohitaji, walimuamuru kutoka nje kwa kuwa ndani alikuwa amelala na mtoto wa jirani yake, wakampeleka kwenye kichochoro kisha wakamfanyia ukatili huo na baadaye kuondoka na nguo zake za ndani.

Mwenyekiti wa mtaa wa Joshoni, Amon Swale amekiri kutokea kwa tukio hilo katika mtaa wake na kusema Serikali ya mtaa imejipanga kuitisha mkutano wa dharura ili kujadili kwa pamoja unyama huo uliotokea.