Vyakula vya kuepuka kwa wagonjwa wa figo

0
15

Wataalamu wanasema vyakula vinavyozuiwa kwa mgonjwa wa figo hutofautiana kulingana na kiwango cha uharibifu wa kiungo hicho.
Akizungumza Ofisa Lishe Mtafiti kutoka taasisi ya chakula na lishe Tanzania (TFNC), Fatma Mwasora anasema kwa watu wenye ugonjwa wa figo wa hali ya juu ni muhimu kufuata ushauri wa lishe unaofaa kwani husaidia uchujaji wa uchafu na utokaji wa maji mwilini, lengo ni kupunguza sumu kwenye damu.

Mtaalamu anasema mgonjwa wa figo anashauriwa kuepukana na matumizi ya vyakula vyenye madini ya sodium ambayo kwa kiwango kikubwa hupatikana kwenye chumvi ya mezani hivyo husababisha kuvimba kwa vifundo vya mguu, shinikizo la damu, shida ya kupumua, mkusanyiko wa maji kuzunguka moyo na mapafu.

Anasema, wagonjwa wa figo wanahitaji kupunguza kwa kiwango kikubwa matumizi ya vyakula vyenye potasiamu kama vile ndizi, parachichi, tikiti maji, asali, zabibu, mboga za majani, maziwa,viazi, vitamu, matango mbaazi, maboga, uyoga na kadhalika ili kuepuka kiwango kikubwa chenye madini hayo kwenye damu.

Aidha, anaeleza wagonjwa hao wanapaswa kuepuka kwa kiasi kikubwa cha madini ya protini mwilini kwani figo zilizoharibiwa haziwezi kuondoa mabaki ya protini iliyopo kwenye damu na tafiti zinaonesha wagonjwa waliofikia hatua ya mwisho, figo hushindwa kufanya kazi hivyo kulazimika kupatiwa matibabu ya kuchuja na kusafisha damu.

“Inabidi mgonjwa apunguze kula vyakula vyenye protini nyingi hasa za wanyama ambazo ni nyama, dagaa na bidhaa za maziwa,“ anasema Daktari.

Chanzo: Mwananchi.