Dereva adaiwa kumuua kondakta wake kisa wivu wa mapenzi

0
14

Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam linamshikilia dereva wa daladala, Maarifa Matala (45) mkazi wa Kimara Suka, Wilaya ya Ubungo kwa tuhuma za kumuua mpenzi wake Sharifa Nyamaishwa (31) aliyekuwa kondakta wa gari hiyo.

Kamanda wa Polisi, Jumanne Muliro amethibitisha kutokea kwa tukio hilo Agosti 16, mwaka huu ambapo marehemu Sharifa mkazi wa Kimara Suka aliuawa kwa kushambuliwa sehemu mbalimbali za mwili wake.

“Baada ya dereva huyu kutenda tukio hili, alikimbia, Sharifa alifariki dunia baadaye. Polisi baada ya kupata taarifa tulifanya upelelezi na ufuatiliaji wa haraka tukamkamata akiwa mkoani Lindi alikojificha,” ameleza Kamanda Muliro.

Kamanda Muliro ameeleza kuwa, uchunguzi wa awali umebaini wapenzi hao walikuwa na migogoro inayosababishwa na wivu wa kimapenzi uliopelekea kugombana mara kwa mara, na kwamba mwili wa marehemu umekutwa na majeraha.