Baraza la michezo lamfutia mashitaka aliyekuwa Mwenyekiti wa Chama cha Mpira wa Miguu

0
17

Wizara kupitia Baraza la Michezo la Taifa (BMT) imemsamehe na kumfutia adhabu zote aliyekuwa Mwenyekiti wa Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Mbeya, Elias Mwanjala.

Mwanjala alipewa adhabu ya kutojishughulisha na shughuli za Uongozi wa Michezo kwa kipindi cha miaka miwili kuanzia Desemba 31, 2020 hadi Desemba 31, 2022.

Msamaha huo umetolewa kufuatia ombi lake aliloliwasilisha wizarani la kuomba kusamehewa, ambapo adhabu hiyo ameitumikia kikamilifu kwa zaidi ya asilimia 85.

Aidha, wizara imefafanua kuwa wanafamilia wa michezo kote nchini wanatakiwa kuwa na moyo wa kuvumiliana na kusameheana ili kutumia uwezo na uzoefu wa kila mmoja katika kushauri na kukuza tasnia ya michezo nchini.

Wizara imewasisitiza wadau na familia ya michezo kuzingatia na kufuata sheria, kanuni, utaratibu na miongozo iliyowekwa ili kuleta na kuchochea ustawi wa maendeleo ya michezo.

Send this to a friend