Mashtaka yanayomkabili aliyekuwa kocha wa makipa Simba, Muharami Sultan na wenzake

0
21

Washtakiwa sita kati ya tisa akiwemo aliyekuwa kocha wa makipa wa Simba SC, Muharami Sultan (40) na wenzake watano wamefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kwa tuhuma za kusafirisha dawa za kulevya aina ya heroine.

Wakisomewa mashtaka hayo Novemba 21, 2022 na wakili wa Serikali Mwandamizi, Grace Mwanga mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Mery Mrio amesema watuhumiwa hao wanakabiliwa na mashtaka mawili ya kusafirisha dawa hizo zenye uzito wa kilo 34.89.

Grace amedai Oktoba 27 mwaka huu eneo la Kivule jijini Dar es Salaam washtakiwa wote kwa pamoja walisafirisha heroine yenye uzito wa kilo 27.1, na shtaka la pili watuhumiwa hao wanadaiwa kusafirisha heroine yenye uzito wa kilo 7.79.

Ameieleza mahakama hiyo kuwa upelelezi wa shauri hilo bado haujakamilika na kuiomba mahakama ipange tarehe nyingine, hata hivyo hakimu amedai mahakama hiyo haina mamlaka ya kusikiliza shauri hilo hivyo washtakiwa hawatakiwi kujibu chochote na kuahirisha kesi hadi Desemba 5.

Watuhumiwa wengine waliofikishwa mahakamani ni mmiliki wa kituo cha Cambiasso Sports Academy, Kambi Seif, Said Matwiko, Maulid Mzungu maarufu Mbonde, John John na Sarah Joseph.

Hata hivyo Mamlaka ya Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA) imesema watuhumiwa wengine hawakufikishwa mahakama kutokana na upelelezi wao kutokamilika.