Fahamu kwanini unapata tatizo la kukosa choo na nini cha kufanya

0
15

Tatizo la kukosa choo kwa muda mrefu, (constipation) huweza kumpata mtu yeyote. Kuna watu wanaopata choo mara tatu kwa siku, wengine hupata mara chache kwa wiki. Kwa wale wanaofika siku tatu bila kupata choo huchukuliwa ni muda mrefu sana hivyo wako katika hatari.

Kuna baadhi ya mambo ambayo huchangia kukosa choo kwa muda mrefu/choo kigumu, na hivi ni baadhi ya vyanzo vinavyoweza kusababisha tatizo hilo;

Msongo wa mawazo
Watu wanaopata msongo mkubwa wa mawazo huharibu mpangilio wa homoni zao pamoja na kuathiri uzalishaji wa visambaza taarifa kwenye mwili, na hivyo kusababisha shida kwenye misuli na kuathiri ufanyaji kazi wa ‘enyzmes’ ambazo husaidia kumeng’enya chakula.

Ubovu wa lishe
Matumizi ya vyakula vilivyosindikwa sana, sukari, nafaka iliyokobolewa, pombe, vyakula vilivyoongezwa sukari na kemikali za kutunza chakula kisiharibike na mafuta mabaya huleta ugumu kwenye utengenezaji na utolewaji wa choo hivyo kusababisha kukosa choo kwa muda mrefu.

Kutoshughulisha mwili
Utafiti unaonesha watu wanaotumia muda mwingi wakiwa wamekaa hasa ofisini wanaongoza kwa kupata matatizo ya kukosa choo kwa mda mrefu. Unashauriwa kufanya mazoezi kwani husaidia kuimarisha mzunguko wa damu kwenye mfumo wa chakula na kuimarisha misuli.

Matumizi ya baadhi ya vidonge
Baadhi ya vidonge husababisha kukosa choo kwa muda mrefu na kupata choo kigumu. Mfano dawa za kupunguza maumivu, dawa za kuondoa msongo wa mawazo, dawa za kulevya, virutubisho vya calcium, magnesium na antiacids.

Matatizo ya tezi ya thyroid na matatizo mengine ya homoni:
Matatizo kama kisukari, kukoma hedhi, maumivu kabla ya hedhi na ufanyaji kazi hafifu wa tezi ya ‘thyroid’ huweza kusababisha kupata shida ya kupata choo. Magonjwa mengine ni kama Pakinson disease, ajali ya uti wa mgongo na matatizo mengine ya neva.

Upungufu wa magnesium
Magnesium husaidia ufanyaji kazi mzuri wa misuli yako, hivyo upungufu wa magnesium unaweza kusababisha tatizo la kukosa choo kwa muda mrefu.

Tabia hatarishi ukiwa chooni
Kuna baadhi ya tabia ambazo ni hatarishi kama kujisaidia kwa haraka na ukaaji mbaya unapokuwa chooni ambazo huchangia kuongeza ukubwa wa tatizo na kuchangia kupata ugonjwa wa bawasili.

Fanya mambo haya yafuatayo ili kuzuia tatizo la kukosa choo kwa muda mrefu;

. Kula zaidi chakula chenye nyuzinyuzi kama maharage, mboga za majani,
matunda, nafaka nzima
. Kunywa maji mengi
. Fanya mazoezi ya mwili
. Jaribu kudhibiti msongo wa mawazo
. Usiahirishe kwenda chooni
. Jaribu kuweka ratiba maalumu ya kujisaidia, hasa baada ya kula.

Send this to a friend