Fursa za ajira laki 5 zimezalishwa nchini

0
21

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa amesema katika mwaka 2022/2023, jumla ya fursa za ajira 547,031 zilizalishwa nchini, kati ya hizo, ajira 321,363 zilizalishwa kupitia Serikali na utekelezaji wa miradi ya maendeleo, na 225,668 kupitia sekta binafsi.

Amesema hayo Bungeni Dodoma wakati akisoma hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Ofisi na Wizara zilizo chini yake ambapo amesema Serikali imeendelea kuratibu masuala ya uzalishaji wa fursa za ajira nchini kupitia utekelezaji wa miradi ya kielelezo, kujenga mazingira wezeshi kwa wawekezaji na kuimarisha ushirikiano baina ya Serikali na sekta binafsi.

Bei ya petroli na dizeli zashuka, hizi ni bei mpya kwa mikoa yote

“Serikali itaendelea kuwezesha na kuratibu masuala ya ukuzaji wa fursa za ajira na kazi za staha kwa kuboresha na kutekeleza Sera, Mikakati na Mipango mbalimbali ya Kitaifa, Kikanda na Kimataifa ili kuhakikisha nguvu kazi ya Taifa inapata fursa za kujiajiri au kuajiriwa ili kuchangia katika maendeleo ya Taifa,” amesema.

Aidha, amesema Serikali imeendelea kuchukua hatua ili kuhakikisha wahitimu wa mafunzo ya ujuzi wanaunganishwa na fursa za kujiajiri ili kumwezesha mhitimu wa mafunzo ya ujuzi kupata sehemu ya uzalishaji yenye viwango vinavyohitajika chini ya usimamizi wa watalaamu wenye uzoefu katika fani husika

Send this to a friend