Ghana yakopa trilioni 7 kutoka IMF ili kukabiliana na mdororo wa kiuchumi

0
14

Ghana ambayo ni mojawapo ya wazalishaji wakubwa wa dhahabu na kakao duniani, inakabiliwa na mdororo mkubwa wa kiuchumi, huku bei ya bidhaa zikipanda kwa wastani wa asilimia 41 katika mwaka uliopita.

Hivi karibuni nchi hiyo imetia saini mkopo kutoka Shirika la Fedha Duniani (IMF) wenye thamani ya dola za Kimarekani bilioni 3 (TZS trilioni 7) katika kipindi cha miaka mitatu ili kusaidia kupunguza matatizo hayo na inatarajiwa kupokea awamu ya kwanza ya dola milioni 600 hivi karibuni.

Ghana ambayo kwa muda mrefu imekuwa ikionekana kuwa mojawapo ya nchi zinazoendeshwa vyema zaidi barani Afrika, imekuwa ikijitahidi kujikwamua kutokana na athari za janga la UVIKO-19 na vita nchini Ukraine.

Nchi 10 za Afrika zinazodaiwa zaidi na China

Licha ya kuwa miongoni mwa wazalishaji wakubwa wa kakao na mzalishaji mkuu wa dhahabu barani Afrika, moja ya matatizo ya msingi ya Ghana ni kutopata mapato ya kutosha kupitia mauzo ya nje ili kulipia kila kitu inachoagiza kutoka nje.

Rais Nana Akufo alikiri kuwa nchi hiyo ilikuwa katika mdororo wa kiuchumi huku wapinzani wakiilaumu serikali kwa kile walichodai kuwa ni usimamizi mbaya wa uchumi, madai ambayo serikali imekanusha.

Ukubwa wa deni la Ghana sasa ni karibu asilimia 90 ya jumla ya thamani ya mwaka ya uchumi wake ambapo Serikali ilishindwa kulipa mikopo yake, na hivyo ilibidi ipange upya deni lake na wakopeshaji ili kupata mkopo wa IMF.

Send this to a friend