Serikali yakanusha taarifa ya ndege ya Tanzania kusafirisha mizigo haramu

0
25

Serikali imekanusha taarifa zilizosambazwa kupitia mtandao wa Myflyright.com kuhusu ndege ya Tanzania ya mizigo aina ya Boeing 767-300F kudaiwa kusafirisha mizigo kwa njia haramu.

Akizungumza na vyombo vya habari Mei 31, 2023 Msemaji Mkuu wa Serikali, Gerson Msigwa amesema taarifa hizo zinazoeleza kuwa ndege hiyo imekumbwa na kashfa ya kusafirisha mizigo haramu, kwa kutumia njia haramu ni za upotoshaji na njia moja wapo ya kurudisha nyuma juhudi za serikali katika kukuza sekta ya anga.

“Ndege yetu aina ya boeing 767-300F ndege ya mizigo bado haijafika Tanzania, ndege hii bado iko mikononi mwa watengenezaji, bado iko Marekani haijafika Tanzania kwa hivyo mtandao huu wa myflyright.com umechapisha taarifa za upotoshaji, naomba zipuuzwe hatujahusika na shughuli kama hiyo,” amesema Msigwa.

UVIKO-19 na vita vya Ukraine vyakwamisha majaribio  ya SGR Dar-Morogoro

Aidha, amesema Serikali kupitia Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi inafuatilia mtandao huo na wote waliohusika ili waweze kuchukuliwa hatua kwa kuiharibia sifa Shirika la Ndege la Tanzania (ATCL).