Mwalimu atoroka baada ya mwanafunzi aliyemchapa kufariki

0
12

Jeshi la Polisi Mkoa wa Kilimanjaro linamtafuta mwalimu wa shule ya Msingi Samanga wilayani Rombo mkoani Kilimanjaro baada ya kuhusishwa na kifo cha mwanafunzi wa darasa la kwanza.

Mwalimu huyo ambaye jina limehifadhiwa anatuhumiwa kuhusika na kifo cha Sistus Kimario, mwenye umri wa miaka 7 ambaye alimchapa viboko na kufariki Julai 17 mwaka huu.

Kamanda wa Polisi, Simon Maigwa, amethibitisha kuwa mwalimu huyo amekimbia baada ya tukio la mwanafunzi huyo.

Kamanda Maigwa amewahakikishia wananchi kuwa Jeshi la Polisi linafanya kila juhudi kumsaka mwalimu huyo ili hatua za kisheria ziweze kuchukuliwa ikiwa ni pamoja na kufanya uchunguzi kubaini mazingira yaliyosababisha kifo cha mwanafunzi huyo.

Aidha, ametoa wito kwa umma kutoa ushirikiano wowote unaoweza kusaidia katika kukamatwa kwa mwalimu huyo ili haki iweze kutendeka.

Send this to a friend