TCD yataja maeneo manne ya kurekebishwa kwenye Katiba kabla ya uchaguzi

0
14

Kituo cha Demokrasia Tanzania (TCD) kimeitaka Serikali kufanya mabadiliko madogo ya Katiba iliyopo ili kuruhusu uwepo wa Tume Huru ya Uchaguzi pamoja na marekebisho mengine ya kikatiba na kuwezesha uchaguzi huru na haki wa mwaka 2024 na mwaka 2025.

Akizungumza leo na waandishi wa habari, Mwenyekiti wa TCD, Prof. Ibrahim Lipumba amesema mabadiliko hayo yanayohitajika yanakaribiana na yale Rais wa Awamu ya Nne, Dkt. Jakaya Kikwete ambapo alikubaliana na viongozi wa TCD mwaka 2014 jijini Dodoma na yalizingatia kuwa mchakato wa kupata Katiba mpya hautakamilika kabla ya Uchaguzi Mkuu wa 2015.

Akibainisha maeneo hayo, TCD imetaka Katiba irekebishwe ili kuwezesha kupatikana tume huru ya uchaguzi itakayosimamia uchaguzi wa Serikali za Mitaa na uchaguzi mkuu, pia TAMISEMI isisimamie uchaguzi wa serikali za mitaa.

Eneo jingine alilotaja ni kuruhusu mgombea binafsi asiyedhaminiwa na chama cha Siasa.

Aidha, eneo jingine ni “Rais atatangazwa kashinda kama atapata zaidi ya asilimia 50 ya kura zote halali zilizopigwa. Ikiwa hakuna mgombea aliyepata zaidi ya asilimia 50 ya kura zote, uchaguzi utarudiwa na utakuwa na wagombea wawili walioongoza kwa kura nyingi.”

Eneo la mwisho lililotajwa na TCD ni kwamba matokeo ya uchaguzi wa Rais yaweze kuhojiwa mahakamani.

Send this to a friend