Serikali yanunua vifaa tiba vya bilioni 14.9 kwa ajili ya majimbo yote 214

0
14

Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu amesema Serikali ya Rais Samia Suluhu Hassan imetoa fedha za nyongeza TZS bilioni 14.9 mwezi Novemba, 2023 za kununua vifaa tiba vitakavyosambazwa katika majimbo yote 214 ya Tanzania Bara ili kuendelea kuboresha huduma za afya ya uzazi, mama na mtoto.

Amesema hayo wakati akizindua usambazaji wa vifaa tiba (nje ya vilivyopangwa kununuliwa kwenye bajeti ya 2023/24) ambapo miongoni mwa vifaa ambavyo amepokea ni pamoja na vitanda vya wagonjwa 3,080; vitanda vya kujifungulia 1,000; magodoro 5,500; mashuka 36,808 pamoja na meza za vitanda 306.

“Tunategemea kupokea vifaa tiba vingine hivi karibuni ambavyo ni vitanda vya kujifungulia (4280), vitanda vya kufanyia uchunguzi (examination table) 4280, mkoba wa vifaa vya kujifungulia (delivery kit) 4280, kabati za vitanda (bed side lockers) 6420 na stendi ya dripu (6420),” amesema Waziri Ummy.

Aidha, Waziri Ummy amesema takwimu zinaonesha asilimia 86 ya wanawake wajawazito Tanzania wanajifungulia katika zahanati, vituo vya afya na hospitali za halmashauri, hivyo vifaa hivyo vitakwenda kusaidia kuboresha huduma za afya ya uzazi, mama na mtoto.

Send this to a friend