Rais Samia: Tunapanda miti kuimarisha mazingira ya nchi

0
13

Katika kuadhimisha kumbukizi ya siku ya kuzaliwa ya Rais Samia Suluhu Hassan, amesema siku hii imeadhimishwa kwa kupanda miti kwa sababu ya kuwepo kwa uharibu mkubwa wa mazingira nchini hasa visiwani Zanzibar.

Ameyasema hayo katika zoezi la upandaji miti lililofanyika katika eneo la Donge Muwanda jimbo la Tumbatu Zanzibar, ambapo ameungana na wananchi wa makundi mbalimbali na kupanda miti 4720 ikiwemo miti 120 ya matunda na kutoa rai kwa wananchi kuitunza miti hiyo ili imee na kuwa na manufaa kwa vizazi vijavyo.

Rais Samia amesema upandaji wa miti kwa wingi pamoja na mikoko kutasaidia kurudisha hali asilia ya bahari na kupunguza kasi ya mmomonyoko wa ardhi.

“Tumeamua kupanda miti kwa sababu mazingira yetu ya Tanzania yameharibika, bahari inakuja juu kwa kasi, kama visiwa tuko hatarini, lakini hata maeneo ambayo siyo ya visiwa walioko Pwani na wenyewe wanaliwa na bahari, kwa hiyo tukipanda miti tukirudisha mikoko kule baharini basi hii hali itapunguza kasi yake,” amesema.

Kwa upande mwingine, Rais Samia amezungumza kwa njia ya simu na Mkuu wa mkoa wa Njombe, Antony Mtaka na kuwataka viongozi wa mkoa huo kuendelea kutoa elimu kwa umma juu ya umuhimu wa lishe bora kwa watoto ili wakue vizuri.

Send this to a friend