Rais Samia awapandisha vyeo maofisa wa Polisi 155

0
18

Rais Samia Suluhu Hassan amewapandisha vyeo maofisa wa Polisi 155 ikiwa ni pamoja na na Makamishna Wasaidizi Waandamizi wa Polisi kuwa Manaibu Kamishna wa Polisi (27) na Makamishna Wasaidizi wa Polisi kuwa Makamishna Wasaidizi Waandamizi wa Polisi (128).

Mkuu wa Jeshi la Polisi Nchini, IGP Camillus Wambura amemshukuru Rais kwa kuwapandisha vyeo idadi kubwa ya maafisa hao akibainisha kuwa idadi hiyo haijawahi kutokea tangu nchi ipate uhuru, huku akieleza kuwa kupandishwa vyeo kwa maofisa hao kutaongeza chachu ya utendaji kazi, kutenda haki, uadilifu na nidhamu.

“Sisi tunaahidi na maafisa hawa walioapa leo wanaahidi kwamba Mheshimiwa Rais atarajie maelekezo yake yote yanakwenda kutekelezwa lakini wananchi kwa ujumla sasa wategemee mabadiliko makubwa ya kiutendaji kutoka kwa maafisa hawa,” amesema IGP Wambura.

Historia ya wakimbizi wa Poland waliokimbilia Tengeru

Naye, Kamishna wa Utawala na Menejimenti ya Rasilimali Watu, CP Susan Kaganda amesema miongoni mwa waliopandishwa vyeo, pia wapo maofisa nane wa kike ambao wamepanda vyeo na kuwa Naibu Makamishna wa Polisi.

Akizungumza kwa niaba ya waliopandishwa vyeo Msemaji wa Jeshi la Polisi, Naibu Kamishna wa Polisi, David Misime amesema kupanda kwao vyeo kutaongeza morali na utimamu zaidi wa akili katika kutekeleza majukumu ya kazi za Polisi.