Rais Samia aipongeza REA kwa kutatua changamoto ya muda mrefu ya umeme

0
30

Rais Samia Suluhu Hassan ameupongeza Wakala wa Nishati Vijijini (REA) kwa kazi nzuri wanayoendelea kuifanya nchini ikiwemo mradi wa Kituo cha cha Kupokea na Kupoza umeme cha Ifakara ambacho kimetatua changamoto ya muda mrefu ya umeme kwa wananchi.

Ametoa pongezi hizo wilayani Kilombero, Mkoa wa Morogoro alipotembelea kituo hicho kilichojengwa na Serikali kupitia REA kwa kushirikiana na Umoja wa Ulaya (EU).

Awali, akitoa maelezo kuhusu mradi huo Naibu Waziri Nishati, Judith Kapinga amemshukuru Rais Samia kwa kuridhia kupitia Wizara ya Nishati kujenga vituo 75 vya kupokea, kupoza na kusambaza umeme ikiwa ni jitihada zake za kuhakikisha wananchi katika maeneo yote wanapata umeme wa uhakika.

“Kabla ya mwaka 2021 nchi ilikuwa ina vituo 61 tu vya kupokea na kupoza umeme, tunakushukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kuridhia ujenzi wa vituo vingine vipya 75,” amesema huku akiongeza kuwa tayari vituo nane vimejengwa na kuanza kazi huku vituo sita vikifikia asilimia 97.

Naye, Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Mhandisi Hassan Saidy amesema gharama ya ujenzi wa kituo hicho ilikuwa TZS bilioni 24.5 ambapo serikali imechangia gharama hizo pamoja na Jumuiya ya Umoja wa Ulaya na kukamilika kwa kituo hicho umesaidia pia kuboresha huduma za kijamii.