Fahamu historia ya Simba Tundu Lissu na jinsi ya kumuona baada ya Kizimkazi

0
60

Kwa mujibu wa taarifa kutoka Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA), mnyama anayezidi kuwa maarufu nchini Tanzania kwa sasa ni ‘Simba Tundu Lissu’ ambaye alizaliwa Dar es Salaam Zoo, nje kidogo ya jijini la Dar es Salaam eneo la Mwasonga, Kigamboni.

Jina la Simba Tundu Lissu lilitolewa na Rais Samia Suluhu Hassan Agosti 24, 2024 wakati akitembelea mabanda ya maonesho yaliyopo Kizimkazi Dimbani Mkoa wa Kusini Unguja, Zanzibar, ambapo Rais Samia alieleza kuwa nia kumpa jina Simba huyo ni kutokana na umachachari wa mwanasiasa ambaye ni Makamu Mwenyekiti wa CHADEMA, Tundu Lissu.

Simba Tundu Lissu alizaliwa Januari Mosi, 2018, hivyo kwa sasa ana miaka 7. Simba huyu ana asili ya Hifadhi mchanganyiko za Mapori ya Akiba ya Grumeti na Ikorongo yanayopatikana katika Mfumo Ikolojia ya Serengeti, Kaskazini mwa Tanzania ambako ndiko wazazi wake walikotokea kabla hawajahamishiwa Dar es Salaam Zoo. Hivyo Simba Tundu Lissu ni ‘born town.’

Tabia za Simba Lissu

Simba Tundu Lissu ni mnyama mwenye tabia za kipekee ikiwemo upole na mwenye urafiki kwa wageni wanaomtembelea katika Bustani ya wanyamapori ya Dar es Salaam Zoo. Mara nyingi hujulikana kwa utulivu wake na anaonekana kufurahia uwepo wa watu wanaomzunguka.

Hata hivyo, kama ilivyo kwa wanyama wa porini, Tundu Lissu ana silika ya kujihami na kwa nadra anaweza kuwa mkali pale anapohisi maisha yake yako hatarini. Tabia hizi zinamfanya kuwa simba wa kuvutia na anayehitaji kuzingatiwa kwa makini katika mazingira yake.

Taarifa ya TAWA inaonesha kuwa baba yake alizaliwa na kuishi Pori la Akiba la Grumeti karibu na Hifadhi ya Taifa ya Serengeti huku mama yake akiwa na asili ya maeneo ya Ushoroba wa Tarangire-Manyara na alifahamika baadaye kwa kuishi eneo lililohifadhiwa la Makuyuni (Makuyuni Wildlife Park).

Je, kuna wanyamapori wengine wenye majina ya viongozi?

Jibu ni ndio, wapo wanyamapori nchini wenye majina ya viongozi na wengine wako katika hatua za mwisho kutangazwa.

Baadhi ambao wapo tayari na wengi wakiwa ni faru ni hawa hapa;

A: Tanapa:

1. Faru Magufuli
2. ⁠Faru Majaliwa
3. Faru Samia (yupo kwenye mchakato wa mwisho)
4. Faru Ummy Mwalimu
5. Faru Janet Magufuli
6. Faru Balozi Regine Hess

B: Ngorongoro:

1. M6 Faru Pius Msekwa
2. M7 Faru Telele
3. M9 Faru Ndugai
4. M10 Faru OBAMA
5. M14 Faru Sokoine
6. M17 Faru Lemanya
7. F31 Faru Hillary Clinton

C: Tawa:

1. Faru Semfuko
2. ⁠Faru Mabula
3. ⁠Faru Gloria

Send this to a friend