Watano wakamatwa kwa kuwaua wanaodaiwa kuwa wezi na kuteketeza miili yao

0
2

Jeshi la Polisi mkoani Simiyu linawashikilia watu watano kwa tuhuma za kuwakamata na kuwaua watu wawili waliojulikana kwa jina la Ntawa Limbu (32) na mwenzake aliyejulikana kwa jina moja la Suma kisha kuteketeza miili yao kwa moto.

Taarifa iliyotolewa na Kamanda wa Polisi mkoani Simiyu, Edith Swebe imeeleza kuwa chanzo cha kufanya uhalifu huo ni kwamba inasemekana marehemu hao walikuwa wanamiliki mali zinazosadikika kuwa ni za wizi na mara baada ya taarifa kumfikia mhanga aliyewahi kuibiwa, alihamasisha kundi la vijana waendesha pikipiki (bodaboda) kuanza kuwatafuta watuhumiwa hao.

“Jeshi la Polisi Mkoa wa Simiyu linaendelea kutoa wito kwa baadhi ya wananchi kuacha tabia za kujichukulia sheria mkononi kwani ni kosa kisheria, Jeshi la Polisi litawakamata na kuwafikisha mahakamani, “ imeeleza.

Aidha, Jeshi la Polisi limesema kwasasa uchunguzi unakamilishwa ili taratibu zingine za kisheria zifuate za kuwafikisha mahakamani.