CHADEMA yalaani kauli ya udini iliyotolewa na wazee wa CHADEMA Zanzibar

0
11

Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kimelaani kauli zilizotolewa zenye viashiria vya udini ambazo zimesikika wakati wazee wa chama hicho walipokuwa wakifanya mkutano na waandishi wa habari Zanzibar.

Mkutano huo ulifanyika Oktoba 01, 2024, ikiwa ni maadhimisho ya Siku ya Wazee Duniani, ambapo walielezea mambo mbalimbali yanayohusu wazee na hali zao za maisha kwa ujumla ikiwemo afya, uchumi na ushiriki wao katika maamuzi.

“Tunajitenga na kauli zote zilizotolewa zenye viashiria vya udini kwani huo sio msimamo wa chama na zinapaswa kupingwa na kila Mtanzania bila kujali dini, kabila au mahali alipotoka,” imeeleza taarifa iliyotolewa na CHADEMA kwa vyombo vya Habari.

Aidha, CHADEMA imesema mamlaka za chama zinazohusika zitafuatilia kiini cha kauli hizo na kuchukua hatua stahiki kwa mujibu wa Katiba, kanuni na miongozo ya Chama.