Adaiwa kuua binti wa kazi na mtoto wa mwalimu aliyemkataa

0
12

Jeshi la Polisi Mkoa wa Katavi linawashikilia watu wawili wakazi wa Kitongoji cha Kabatini Kijiji cha Mpembe Wilaya ya Tanganyika Mkoa wa Katavi kwa tuhuma za kuwaua kikatili watoto wawili kwa kuwakata kata kwa mapanga kwa madai ya kukataliwa kimapenzi.

Akizungumzia tukio hilo Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Katavi, Kaster Ngonyani amewataja watuhumiwa hao kuwa ni Dotto Machia (37) na Kija Maige (25) wote wakazi wa Kitongoji cha Kabatini, ambao mmoja wa watuhumiwa alimpenda mwalimu anayefahamika kwa jina la Rose lakini mwalimu huyo alimkataa ndipo aliamua kulipa kisasi.

Kamanda Ngonyani ameeleza kuwa kutokana na mwanaume huyo kukataliwa, aliamua kukodi mtu na kumlipa shilingi 400,000 ili kumuua walimu huyo kwa madai kuwa amekula fedha zake nyingi bila mafanikio.

“Mtuhumiwa alipokea zile fedha baada ya kufika nyumbani kwa mwalimu hakumkuta, akaamua kuingia ndani kuiba chochote cha thamani, baada ya msaidizi wa ndani kupiga kelele, akaamua kumkata panga yeye na mtoto,” ameeleza.

Kamanda Ngonyani amewataja watoto waliouawa kuwa ni Mariamu Mtimvi (13) na Ester Zuberi Enock (2) huku uchunguzi zaidi wa tukio hilo ukiendelea, na mara utakapokuwa umekamilika watuhumiwa watafikishwa mahakamani ili kujibu tuhuma zinazowakabili.

Send this to a friend