Adhabu tatu zitakazomkabili Wankyo Nyigesa akitiwa hatiani

0
25

Aliyekuwa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kagera, Wankyo Nyigesa huenda akakabiliwa na adhabu ya kuvuliwa cheo chake, kustaafishwa au kupewa onyo endapo Mkuu wa Jeshi la Polisi (IGP) atatoa mapendekezo hayo kwa Amiri Jeshi Mkuu na Rais wa Tanzania.

Hayo yamesemwa na baadhi ya maofisa wa polisi walioko kazini na waliostaafu kufuatia kauli ya ACP Wankyo kudai kutamani Ukuu wa jeshi la polisi na kubainisha kuwa amedharau mamlaka ya kiongozi wake, IGP, na pia kudharau cheo cha Rais.

“Ukimsikiliza anaomba ateuliwe kuwa IGP halafu anasema atafanya mambo makubwa zaidi. Tafsiri yangu mimi ni kwamba alikuwa anamsema indirect [sio moja kwa moja] IGP ambaye ni bosi wake kuwa hafanyi vizuri,” amesema mmoja wa maofisa.

RPC Kagera aliyesema anataka kuwa IGP arejeshwa Makao Makuu ya Polisi, Dodoma

Wankyo alitamka hadharani matamanio yake ya kuwa IGP katika hafla ya kumuaga iliyofanyika Kibaha mkoani Pwani na kumuomba Rais siku moja amteue kuwa IGP na kumuahidi kufanya vizuri zaidi.

“Mimi naamini nitafanya makubwa, huwa ninaomba sana Mama siku moja aniote tu halafu anitamke tu niwe IGP, mimi nitamuomba nifanye miaka mitatu halafu nimwambie mama nakukabidhi naondoka, unaonaje hapo?” alisema Wankyo.

Hata hivyo Jeshi la Polisi kupitia msemaji wake David Misime, lilitoa taarifa kwa vyombo vya Habari kuwepo mabadiliko ambayo yamemtoa Wankyo katika wadhifa wake wa wa RPC na kurudishwa makao makuu ya jeshi Dodoma kwa ajili ya uchunguzi.

Chanzo: Mwananchi