Agizo jipya la Waziri Nape kwa TCRA na kampuni za simu kuhusu bando

0
14

Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Nape Nnauye ameilekeza Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania TCRA na makampuni ya simu kutatua malalamiko ya matumizi ya bando ambayo mtumiaji hajui limetumikaje.

Akizungumza hayo Jijini Dodoma wakati akipokea taarifa ya tathmini ya hali ya mawasiliano amemtaka kila mtoa huduma ya mawasiliano aende kwa wateja wake pamoja na wadau wanaowasaidia kutoa huduma kwa wananchi ili wasikilize malalamiko na kuyatatua.

Aidha, ameelekeza makampuni ya simu kuboresha programu tumizi (mobile application) ili iwe rahisi kuisoma na itoe taarifa nyingi zaidi kuepusha malalamiko ya watu kutokujua wametumiaje data zao.

Katika hatua nyingine, Waziri ameitaka TCRA na makampuni ya simu kuona namna ya kumsaidia kila mtanzania kumiliki na kutumia simu janja kwa kuangalia namna ya upatikanaji wa simu janja kwa bei nafuu.