Agizo la RC Makalla kwa Machinga wanaorudi barabarani

0
16

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Amos Makalla ametoa onyo kwa Wafanyabiashara wanaoendelea kufanya biashara pembezoni mwa Barabara ya Airport licha ya vibanda vyao kuondolewa, na amewataka kuhama mara moja na kwenda kwenye maeneo yaliyotengwa.

Makalla ametoa onyo hilo mapema leo alipotembea mguu kwa mguu kutoka Airport hadi Chang’ombe kuona utekelezaji wa maelekezo ya Serikali ambapo ameshuhudia baadha ya Wafanyabiashara wakijiiba na kupika vyakula chini ya miti na kuwataka waondoke na kwenda kwenye maeneo yaliyotengwa.

Aidha, amesema kuvunja kibanda na kuendelea kupika chini ni kazi bure hivyo amewaelekeza wakurugenzi, watendaji wa kata na mitaa kuhakikisha wanasimamia wafanyabiashara hao wasirudi upya.

Makalla amesema kwa unyeti wa Barabara ya Airport atahakikisha anasimamia Barabara hiyo iwe na mandhari nzuri.

Pamoja na hayo amesema zoezi hilo ni endelevu na ifikapo Novemba 6 mkoa utazindua kampeni ya usafi wa mazingira hivyo amewataka wenye ndoto ya kurudi kwenye maeneo yaliyokatazwa wasahau suala hilo.

Send this to a friend