Ahadi ya Jecha Salim Jecha baada ya kuchukua fomu ya Urais Zanzibar

0
15

Aliyewahi kuwa Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar, Jecha Salum Jecha leo Juni 20 amechukua fomu kuomba ridhaa ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), kuwania nafasi ya #UraisZanzibar2020.

Jecha ambaye ndiye alikuwa akiongoza tume ya uchaguzi wakati ilipobatilisha mchakato wa uchaguzi mkuu mwaka 2015 visiwani humo amechukua fomu katika Afisi za CCM zilizopo Kisiwandui, Unguja.

Akizungumza baada ya zoezi hilo amesema kuwa endapo atapewa ridhaa ya kugombea, atahakikisha anawaunganisha wananchi wote wa Zanzibar.

“Madhumuni yangu makubwa kama nitapata ridhaa ya Chama cha Mapinduzi wakinipendekeza kugombea ni kuwaunganisha wananchi wote wa Zanzibar na Watanzania kwa ujumla katika shughuli za maendeleo, shughuli za kijamii na shughuli nyinginezo,” amesema Jecha.

Amebainisha kuwa atasimamia haki za wananchi wote bila kujali utofauti wao wa dini, rangi, kabila, itikadi za kisiasa wala mtu anapotoka.

“Watu wote kwangu mimi ni sawa. Na nitawaheshimu wote na nitakaribisha maoni ya maendeleo,” amejinasibu mtia nia huyo.

Juni 20, 2018, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Ali Mohammed Shein alimteua Jaji Mkuu Mstaafu, Hamid Mahmoud Hamid kuwa Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar, akichukua nafasi ya Jecha Salim Jecha.

Send this to a friend