Ahukumiwa jela maisha kwa kumlawiti mtoto wa dada yake

0
13

Mahakama ya Hakimu Mkazi Wilaya ya Iringa imemuhukumu kifungo cha maisha na fidia ya TZS milioni 10 Ramadhan Musa Chewa (34) mkazi wa Pawaga kwa kosa la kumuingilia kinyume na maumbile mtoto wa kike wa dada yake mwenye umri wa miaka 12, mwanafunzi wa darasa la nne katika Shule ya Msingi M-boliboli.

Akitoa hukumu hiyo Hakimu wa Mahakama hiyo, Said Ally Mkasiwa amesema mtuhumiwa alitenda kosa hilo April 4, 2020 alipokwenda kumsalimia dada yake.

Imeelezwa kuwa mtuhumiwa alikuwa akilala sebuleni na ilipofika siku ya tatu dada yake alikwenda kuchota maji asubuhi ndipo mtuhumiwa akaingia chumbani alipokuwa amelala mtoto huyo na kumlawiti.

Aidha, Mwendesha Mashtaka wa Serikali, Nashon Saimon aliiomba mahakama kutoa adhabu kali kutokana na mtoto kufanyiwa kitendo kisicho na maadili cha kuingiliwa kinyume na maumbile, pamoja na kitendo hicho kumwathiri kisaikolojia na kimaumbile.

Kwa upande wa mtuhumiwa alipopewa nafasi ya kujitetea aliiomba mahakama impe msamaha wa kifungo, na upande wa fidia alisema atamfidia mwathirika shamba lake la heka moja lililopo eneo la Pawaga, hata hivyo mahakama ilitupilia mbali ombi la mtuhumiwa baada ya kumkuta na hatia.

Send this to a friend