Alichoandika Tundu Lissu baada ya kesi yake kufutwa

0
10

Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu leo imeifuta kesi ya uchochezi iliyokuwa inamkabili, Makamu Mwenyekiti wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleao (CHADEMA) Tanzania Bara, Tundu Lissu na wenzake watatu.

Mahakama imefikia uamuzi huo baada ya Mkurugenzi wa Mashtaka nchini Tanzania (DPP) kuieleza kuwa hana nia ya kuendelea na mashtaka dhidi yao.

Baada ya taarifa hiyo, Tundu Lissu kupitia ukurasa wake wa Twitter ametaka pia kesi nyingine zinazomkabili yenye na viongozi wengine wa CHADEMA zifutwe, kwa maelezo kuwa ni za uongo.

“Baada ya kutusumbua kwa miaka 5 kwa kesi ya uongo ya uchochezi, DPP ameifuta kesi hiyo. Lakini bado kuna kesi nyingine 5 za uongo dhidi yangu & mamia nyingine dhidi ya viongozi, wanachama & Mwenyekiti wetu Freeman Mbowe. Zote hizo zinatakiwa kufutwa bila masharti yoyote,” ameandika Lissu.

Lissu na wenzake walikuwa wanakabiliwa na mashtaka matano likiwemo la kuandika habari za uchochezi kinyume na Sheria ya Magazeti ya Mwaka 2002, katika kesi ya jinai namba 208/2016.


Mbali na Lissu, washtakiwa wengine katika kesi hiyo ni Jabir Idris, Mhariri wa Gazeti la Mawio, Simon Mkina, Mchapishaji wa Kampuni ya Jamana, Ismail Mehboo.

Send this to a friend