Ally Kamwe, Mazanzala waitwa Kamati ya Maadili TFF

0
13

Kamati ya Uendeshaji na Usimamizi wa Ligi imewapeleka kwenye Kamati ya Maadili ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Afisa Habari wa Yanga SC, Ally Kamwe na Afisa Habari wa klabu ya Kagera Sugar, Hamis Mazanzala kwa tuhuma za kutenda makosa ya kimaadili.

Taarifa iliyotolewa na Bodi ya Ligi Kuu imesema maafisa hao wamedaiwa kutenda kosa hilo kupitia machapisho yao kwenye kurasa za mtandao wa kijamii wa Instagram.

“Viongozi na maafisa wa klabu wanazuiliwa kwa mujibu wa kanuni kutoa maandiko au matamshi chonganishi ama yanayoweza kuchafua taswira ya ligi na mpira wa miguu kwa ujumla,” imeeleza taarifa.

Aidha, Bodi imewakumbusha maafisa Habari na wasemaji wa klabu zote kuzingatia kanuni za Ligi na za maadili katika majukumu yao ili kuepuka kauli zinazoweza kuzua chuki, taharuki au kuchochea vurugu viwanjani.