Ashtakiwa kwa kukutwa na sehemu tano za siri za wanawake

0
11

Salum Nkonja mkazi wa Maswa Simiyu amepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kwa madai ya uhujumu uchumi yenye mashtaka 11 ikiwemo kukutwa na sehemu tano za siri za kike.

Mshtakiwa huyo amekutwa na chuchu tano za wanawake, mafuvu mawili ya binadamu pamoja na sehemu za siri za wanyama.

Akisoma mashtaka hayo mbele ya Hakimu Mkazi Mwandamizi, Ramadhani Rugemalira, Wakili wa Serikali Carolina Matemu amedai Oktoba 30, 2017 wilayani Ubongo, Dar es salaam, mtuhumiwa alikutwa na sikio na pembe ya nyati  vikiwa na zaidi ya thamani ya shilingi milioni nne bila kibali kutoka kwa mkurugenzi wa wanyamapori.

Ameongeza kuwa katika tarehe na eno hilo, mshtakiwa alikutwa na uume wa mbwamwitu wenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni 2.2 pamoja na uume wa nyumbu wenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni 1.8.

Mbali na hayo Matemu amedai mshtakiwa alikutwa pia na mikia mitano ya ngiri, uume mitatu ya fisi, yai moja la mbuni, ngozi ya Ngekewa, kichwa kimoja cha nyoka aina ya kobra chenye thamani ya zaidi ya shilingi laki moja.

Mshtakiwa amekana mashtaka hayo, huku upande wa mashtaka ukidai upelelezi umekamilika na kuomba tarehe nyingine ya kumsomea mshtakiwa hoja za awali.

Kesi hiyo itasikilizwa tena Julai 5, 2022 na mshtakiwa amerudishwa mahabusu baada ya kukosa wadhamini.