Baba amshitaki mwanae mahakamani kwa kutompa fedha ya matunzo

0
12

Baba mzazi amemshitaki mwanae wa kiume mahakama akitaka kulipwa asilimia 20 ya mshahara wake kila mwezi kama sehemu ya matunzo.

Gideon Kisira Cherowo (73) amesema kwamba aliuza shamba lake na mali nyinginezo kulipia gharama za shule za mwanae hadi alipofika chuo kikuu, akitegemea atamsadia baadaye.

Mzee Cherowo amesema kuwa mtoto wake huyo ambaye sasa ana umri wa miaka 48 hamsaidii kumudu gharama za maisha.

Mtoto huyo ni wapili kati ya watoto wanne wa Mzee Cherowo na ndiye pekee aliyeajiriwa serikalini ambapo anafanya kazi Mamlaka ya Viwanja wa Ndege Kenya.

Amedai kuwa mtoto huyo hajafika nyumbani kwa miaka 17 na hakuna msaada anaotoa licha ya maombi ya familia yake.

Akiwa mahakamani hapo ameiambia mahakama kwamba hawezi kumudu gharama za mwanasheria, na amekwenda na mtoto wake wa mwisho kama shahidi.

Mtoto huyo amesema kaka yake aliwatelekeza baada ya kupata kazi jijini Nairobi ambapo wao wanaishi kwenye nyumba ya tope Magharibi mwa Kenya.

Baada ya kutoka mahakamani hapo amesema familia imekubaliana kukutana Jumatatu kuzungumzia suala hilo na kwamba anatamani jambo hilo limalizike nje ya mahakama.

Send this to a friend