Balozi Karume afutwa uanachama CCM

0
12

Halmshauri Kuu Chama Cha Mapinduzi (CCM) mkoa wa Kusini Unguja imemfuta uanachama kada wake, Balozi Ali Karume baada ya kutangaza kumuweka chini ya uangalizi kutokana na kauli zake za kukidhalilisha chama na viongozi wake.

Kikao cha kumfuta uanachama Balozi Karume kimefanyika saa saba usiku wa kuamkia leo Jumamosi Julai 8, 2023 chini ya Katibu wa Mkoa wa CCM, Amina Mnacho.

Taarifa ya kumwondosha kwenye chama hicho ilitolewa na Katibu Mwenezi wa Mkoa huo, Ali Timamu Haji.

Hatua hiyo inatokana na onyo alilopewa na kamati ya siasa ya Halmashauri Kuu ya CCM Jimbo la Tunguu, Mkoa wa Kusini Unguja iliyokutana Juni 15 mwaka huu.

Karume aliitwa kuhojiwa na kamati ya maadili ya jimbo hilo kutokana na kauli zake alizozitoa kwenye mitandao ya kijamii, akikituhumu chama kuwa hakijawahi kushinda kihalali kisiwani humo na kumkosoa hadharani Rais Hussein Mwinyi kuhusu sera zake za kukodisha visiwa.

Send this to a friend