Balozi Paul Rupia, mtoto wa mpigania uhuru, afariki dunia

0
19

Katibu Mkuu Kiongozi wa tano, Balozi Paul Rupia (84) amefariki dunia leo asubuhi Septemba 16, 2022 nchini Afrika Kusini wakati akipatiwa matibabu.

Balozi Rupia ambaye ni mtoto wa mpigania uhuru, mfanyabiashara na mwanasiasa, John Rupia, amewahi kuwa Ofisa katika Wizara ya Mambo ya Nje kuanzia mwaka 1963 na baadaye alikuwa balozi wa Tanzania katika nchi mbalimbali ikiwamo Uingereza na balozi wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa.

Pia, aliwahi kuwa Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, na Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Benki ya Watu wa Dar es Salaam.

Baba yake balozi Rupia (John Rupia) anatajwa kuwa ndiye aliyekuwa mfadhili namba moja kwa kukiendesha na kukikuza chama cha TANU kwa kujitolea kulipa mishahara na posho, pia aligharamia safari ya Mwalimu Nyerere kwenda Umoja wa Mataifa kuelezea dunia kwamba Watanganyika walikuwa tayari kujitawala.

Balozi Rupia ameacha mjane, Rose Rupia na watoto wanne Peter, Suzan, Pauline na Simon.

Send this to a friend