Benki ya Dunia yabaini makosa kwenye ripoti za viwango vya ufanyaji biashara

0
14

Benki ya Dunia (WB) imetangaza kusitisha kutoa ripoti ya viwango vya urahisi wa ufanyaji wa biashara (Doing Business Report) ambazo zimekuwa zikiagalia urahisi wa ufanyaji wa biashara na uwekezaji kwenye nchi mbalimbali.

Taasisi hiyo ya kifedha imefikia umauzi huo baada ya kubaini uwepo wa makosa ya kitakwimu katika ripoti ya mwaka 2018 na mwaka 2020. Mwaka 2020 benki hiyo ilizuia kutolewa kwa ripoti ya baada kubainika kuwepo kwa makosa ya takwimu.

Baadaye WB ilieleza kwamba mabadiliko ya takwimu hizo hayakuwa yakiendana na utaratibu (methodology) wa ripoti ya ufanyaji biashara. Katika taarifa yake imeeleza kwa mfumo/utaratibu mpya utatumika kuweza kuchambua mazingira ya ufanyaji biashara na uwekezaji baada ya makosa yaliyobainika kuibua masuala ya kimaadili yanayowahusisha waliokuwa watumishi wa benki na maafisa wa bodi.

Makosa hayo yaliathiri nchi nne, China, Saudi Arabia, Falme za Kiarabu (UAE), na Azerbaijan. Kwa mujibu wa taarifa ya awali mwaka 2018, China ilipata alama 65.3 na kushika nafasi ya 78 duniani, sawa na mwaka 2017. Baada ya masahihisho kwenye takwimu kama kuanzisha biashara, kupata mikopo, na kulipa kodi, China ilianguka hadi alama 64.5, na nafasi yake duniani kushuka hadi 85.

Send this to a friend