Biashara 5 unazoweza kuanzisha kwa mtaji wa TZS 50,000

0
46

Kuanzisha biashara yoyote ile kunahitaji mipango mizuri, ubora katika utoaji huduma, kuelewa mahitaji ya soko lako pamoja na kufanya utafiti juu ya biashara unayotaka kufanya.

Unaweza kuanzisha biashara na ikafanikiwa ikiwa utaweka mikakati mizuri hata kama utaanza kwa mtaji mdogo.

Hizi ni biashara 5 unazoweza kufanya kwa mtaji wa shilingi 50,000;

Kuuza Bidhaa Mtandaoni
Unaweza kuanzisha biashara ya mtandaoni na kutumia mitandao ya kijamii kuuza bidhaa kama nguo, viatu urembo au vitu vingine vyovyote vyenye soko. Hutohitaji kununua mzigo mkubwa, bali cha msingi ni wewe kuwa na picha za bidhaa ambazo utazituma mtandaoni, kwa mtaji ulionao, utaweza kufanya manunuzi madogo na kuuza kwa kila mteja atakayehitaji huku ukiongeza faida yako.

Nguo za Mitumba
Yapo masoko mengi ambayo huuza nguo nyingi za mtumba kwa bei nafuu. Watu wengi hupendelea nguo hizo, hivyo ni rahisi kupata wateja kwa urahisi. Unaweza kutumia maeneo kama vyuoni na mitaani, cha msingi ni kujua aina ya watu na aina za nguo wanazohitaji.

Kutengeneza Sabuni za Maji
Unaweza kutumia sehemu ya mtaji wako kununua vifaa vya kutengenezea sabuni za maji na kuzisambaza kwenye maduka ya rejareja au kwa watu binafsi. Usiwaze kuhusu utengenezaji, unaweza kujifunza mtandaoni au semina mbalimbali ambazo hufundisha ujuzi huo.

Biashara 5 ambazo hupaswi kufanya ukiwa na mtaji mdogo

Huduma ya Usafi
Unaweza kuanzisha biashara ya kutoa huduma ya usafi wa nyumba au ofisi. Anza kwa kununua vifaa vya usafi kama ndoo, madekio, na sabuni za kusafishia, kisha tengeneza ukurasa kwenye mitandao ya kijamii na uwatangazie wafuasi wako kuwa unafanya usafi majumbani na ofisini. Kwa kufanya hivyo utapata watu watakaohitaji huduma hiyo hususani wafanyakazi.

Uchomaji wa Mishikaki
Biashara ya uchomaji wa mishikaki ni maarufu sana. Unaweza kuanza na chombo cha kuchomea mishikaki na nyama, na kuuza kwenye vituo vya barabarani au sehemu zenye shughuli za burudani.

Send this to a friend