Binti amnyonga mwanaye wa miezi tisa ili aende kuishi Dar es Salaam

0
16

Jeshi la Polisi mkoani Iringa linamshikilia Johari Mbuma (19) mkazi wa Mawelewele, Kata ya Mwangata, Halmashauri ya Manispaa ya Iringa kwa tuhuma za kumnyonga hadi kumuua mtoto wake mwenye umri wa miezi tisa ili aende Dar es Salaam kwa mama yake mzazi.

Akieleza sababu za kutenda kosa hilo, amesema amekuwa akiishi maisha magumu na baada ya kuwasiliana na mama yake alikubali ombi lake la kwenda kuishi naye Dar es Salaam lakini kwa sharti la kuwa peke yake bila mwanaye.

“Mama alisema kwa kuwa nimekatisha masomo kwa sababu ya ujauzito na ninataka kwenda kuishi naye Dar es Salaam, basi niende mwenyewe bila mtoto na kama nitakwenda na mtoto nisifikie nyumbani kwake, ndio maana nikalazimika kumnyonga mtoto wangu na kumtupa kwenye ndoo ya maji ili nisafiri kwenda kuishi na mama Dar es Salaam,” ameeleza.

Amesema alitaka kumtelekeza mtoto wake huyo kwa rafiki yake kabla hajapata wazo la kumuua lakini siku ya kutekeleza wazo hilo hakumkuta rafiki yake nyumbani kwake.

Aidha, amesema kuwa baba wa mtoto alimtelekeza mara baada ya kusikia ana ujauzito na wala hajawahi kuwasiliana naye au kutoa huduma kwa mtoto wake.