DIB yasema ina fidia za bilioni 2.9 ambazo wahusika hawajazidai

0
20

Bodi ya Bima ya Amana (DIB) imesema jumla ya fidia ya shilingi bilioni 2.9 hazijachukuliwa na wadai mbalimbali wa benki zilizofilisika nchini tangu mwaka 2000.

Akizungumza na Swahili Times, Meneja Ushirikiano wa Huduma DIB, Rashid Mrutu amesema kiasi kinachotolewa kwa wanaodai benki hizo ni kwa wale ambao thamani zao hazizidi shilingi milioni 1.5 wakati benki hizo zilipofungwa.

“Sheria inasema mabenki yote yaliyopewa lesni na Benki Kuu kufanya biashara ni wanachama wa Deposit Insurance Fund (Mfuko wa Bima ya Amana), kwahiyo wanachangia kwenye mfuko. Benki inapoanguka sisi tunawarejeshea wateja hela, lakini hatuna uwezo wa kuwarejeshea zote.

Kwahiyo mpaka mwezi Februari mwaka huu tulikuwa tuna uwezo wa kuwarejeshea hadi shilingi milioni 1.5 ukizidi hapo nenda kwenye zoezi lingine la ufilisi,” ameeleza.

Waziri Nchemba: Majaribio ya reli ya SGR kuanza Desemba

Ameongeza kuwa mwitikio wa watu kuja kuchukua fidia hizo si mkubwa kutokana na wengine kuwa na kesi mahakamani zinazohusu fedha zao, wengine kuwa nje ya nchi na wengine kuwa na kiasi kidogo cha fedha ambacho hukipuuzia.

Benki ambazo zimefungwa ni Greenland Bank Tanzania Limited (2000), Delphis Bank Tanzania Limited (2003), FBME Bank (2017), Mbinga Community Bank Plc (2017), Njombe Community Bank Limited (2018), Meru Community Bank Limited (2018), Covenant Bank for Women (T) Limited (2018), Kagera Farmers’ Cooperative Bank Limited (2018), na Efatha Bank Limited (2018).