Dkt. Slaa: Hakuna sababu ya Mdee na wenzake 18 kuwepo bungeni

0
15

Aliyekuwa Balozi wa Tanzania nchini Sweden Dkt. Wilbroad Slaa amesema haoni sababu inayowafanya wabunge 19 wanaoongozwa na Halima Mdee kuendelea kuwepo bungeni ilihali chama cha killishafanya uamuzi dhidi yao.

Akizungumza na Nipashe, Slaa amesema wabunge hao hawapaswi kuwepo bungeni kwa kuwa hawana ridhaa ya chama na hakuna zuio la kisheria la kuwafanya kuendelea kuitwa wabunge wa viti maalum.

Katika mazungumzo yake amesema anatambua uwezo wa baadhi ya wabunge hao akiwatolea mfano Mdee, Ester Bulaya na Esther Matiko kwamba alishiriki kuwajenga na kueleza kuwa ni kazi kubwa kujenga wengine wa mfano wa hao.

“Kwa muda mrefu nimekuwa ninakwepa kujibu hili swali kuhusu kina Halima Mdee. Sababu ya kutojibu ni kwamba mimi kichwani kwangu ninashindwa kuamini kwamba wale wanawake wameenda bila mtu fulani kupeleka majina. Kwahiyo nilikuwa ninatafuta, pili kwamba huenda walizungukana huko ndani [CHADEMA].

Nikawa pia ninashindwa kumbana spika kwa sababu kwa kawaida yeye anapeleka majina NEC kwahiyo nikategemea katika kipindi chote wanabishana atajitokeza mtu aseme kuna aliyeghushi, lakini hakuna aliyejitokeza. Nikategemea atajitokeza wa kusema tume haikupeleka majina lakini hakuna,” amesema.

“Spika ametafuta tu kisingizio, watu wasioelewa wanaamini kwa kuwa kuna kesi iliyopo mahakamani lakini wanashindwa kuunganisha ile kesi ni ya nini, ile kesi unataka tu wao kurudishiwa nafasi ya kwenda kusikilizwa, sasa hiyo inahusiana nini na wao kuwepo bungeni?” amehoji.

Send this to a friend